HISTORIA/SHUJAA : JOSINA MACHEL, AFRIKA NA UAFRIKA VOL 1

Kwakua tumetoka kwenye wiki ya mama duniani, niliona si vibaya nikifululiza habari za wanawake katika thread zangu. Kabla wenzangu hawajanijia juu, leo naomba niwape ya dada huyu. Usiongee maneno ya kumdharau kwa mwanamke kabla haujayasikia ya mwanadada Josina Muthemba Machel. Mama wa Taifa la Msumbiji.



Alipambana hasa kuifanya nchi yake ipate uhuru lakini uhuru wenyewe hakuuona. Josina alifariki dunia Aprili 7, 1971, ikiwa ni miaka minne kabla ya nchi hiyo kupata uhuru wake mwaka 1975.

Jina lake ni jina muhimu katika historia ya Msumbiji. Ni kama watanzania wanavyomtaja Bibi Titi. Lakini jasho na machozi ya Bibi Titi, vimeishia kwenye kipande cha barabara kutoka Mnazi Mmoja mpaka makutano ya Barabara ya Ali Hassan Mwinyi na Ohio. Kipande hicho kinaitwa barabara ya Bibi Titi. Eti hiyo tu ndiyo heshima yake pekee kwa mengi aliyofanya. Kuna mwenzangu alizungumza maneno haya na sio mimi

Turudi kwa dada yetu Josina na hayo mengine tutayajadili baadae. Ni mwanadada aliyethubutu kushika silaha dhidi ya utawala wa Kikoloni wa kireno akiwahamasisha wanawake wengine pamoja na wanaume kuingia vitani kudai uhuru.

Josina Muthemba ambaye baada ya kufunga ndoa aliitwa Josina Machel. Aliolewa  na mwanamapinduzi na aliyekuwa rais wa kwanza wa msumbiji SAMORA MACHEL. Josina Alizaliwa akiwa pacha na mwenzake Belmiro Muthemba Agosti 10, 1945 Kusini mwa Msumbiji kwenye mji wa Vilanculos, Inhambane. Wakilelewa na babu ambaye alikua muinjilisti na baba ambaye alifanya kazi kama muuguzi katika hospitali mbalimbali za serikali.

Alipata kuingia shuleni akiwa na umri wa miaka 7, Masomo yake alianzia kwenye mji wa Mociboa da Praia, uliopo Kaskazini ya Msumbiji, baadaye alihamia kwa bibi yake, Mji Mkuu wa nchi hiyo, Lourenco Marques ambao kwa sasa unaitwa Maputo.

Familia ya Josina ilikuwa ikipata upendeleo maalum kutoka kwa wakoloni lakini hilo halikuifanya familia yake iwasaliti raia wenzao. Mfumo huo uliitwa Assimilados kwa kireno na kingereza assimilation.

Baada ya kufkisha miaka 13 alifanikiwa kusoma elimu ya sekondari katika shule ya biashara ambapo alijiunga na Umoja wa Wanafunzi wa Sekondari nchini Msumbiji (NESAM) ambao Mondlane alisaidia kuujenga mwaka 1949. Ni umoja ambao ulilenga kukuza wanafunzi kifikra na kuwajengea uzalendo na moyo wa kuitetea nchi yao.

Baada ya miaka mitano alifaanya jaribio la kwanza la kutoroka Msumbiji ili kujiunga na chama cha ukombozi wa nchi hiyo, FRELIMO, nchini Tanzania. Miongoni mwa watu waliotoroka na Josina ni aliyewahi kuwa rais wa msumbiji , Armando Guebuza.


Baada ya kutembea kwa kwa umbali wa maili 800, Josina na wenzake walikamatwa na wakoloni wa Uingereza katika eneo la Maporomoko ya Victoria Zimbabwe, kisha wakarejeshwa Msumbiji kwa wakoloni wa Kireno, mjini Maputo. Alikaa jela na kutoka baada ya miezi mi 5 na kuruhusiwa kuendelea na masomo yake ya sekondari lakini kwa uangalizi mkubwa wa askari.

Kwakua alikua mdogo (miaka 19) walimdharau na kuona hawezi fanya lolote hivyo wakamwacha. Akafanikiwa kutoroka tena akiwa na wanafunzi wenzake. Safari hii walifika mpaka Swaziland na kupokelewa na baadhi ya wasamaria katika kambi ya wakimbizi. Walitoroka tena Swaziland yeye na wenzake watatu baada ya kupata taarifa kuwa wanataka kurudishwa kwenye mikono ya wareno.

Walisafiri kwa gari na sehem zingine walitembea kwa miguu mpaka wakafika Johannesburg South Afrika. Baadaye kikundi hicho kilisafiri kwa lori kwenda Francistown, Botswana ambapo walijiunga na wengine 14 ambao pia walikua na lengo la kufika Tanzania. Walikamatwa kama wazamiaji na serikali ya uingereza, lakini Mondlane akiwa Rais wa Frelimo aliwapambania mpaka wakakubaliwa kusafiri mpaka Tanzania.

Baada ya safari ndefu na ngumu katika mabasi ya umma, kundi hilo lilifika jijini Dar es salaam, Tanzania. Josina alisafiri karibu maili 2,000 kutoka nyumbani kwake.

Josina akiwa na umri wa miaka 20, aliteuliwa kuwa msaidizi wa mkurugenzi wa Taasisi ya Msumbiji jijini Dar es Salaam. Taasisi iliyojikita na masuala ya elimu chini ya mkurugenzi mkuu mama Janet Mondlane, mwanamke wa Kimarekani, aliyekuwa mke wa Mondalne.
Josiana aliikataa nafasi ya kujiunga na chuo kikuu nchini Swaziland na kukubali kujitolea katika taasisi mpya iliyoanzishwa na FRELIMO  taasisi ya Women’s Detachment. Ikiwa na Lengo la kuwahamasisha wanawake kuunga mkono harakati za ukombozi wa nchi ya Msumbiji.

Mwaka 1967 akiwa mjumbe wa Kamati Kuu ya FRELIMO, alikuwa mmoja kati ya wanawake waliokwenda Nachingwea mkoani Lindi kusini mwa Tanzania katika kambi ya mafunzo ya kijeshi. Samora Machel, rais wa kwanza wa Msumbiji na mume wa baadaye wa Josina alisimama kama mkurugenzi mkuu wa kituo hiko .

Josina aliifanya kazi ya kuhubiri matumaini na kuwahamasisha wananchi kulipigania taifa lao. Alipita kwenye majimbo na kuhamasisha watu hasa vijana, vilevile alipita kanda za ukombozi na kuhudumia majeruhi.

Mwaka 1968, Josina aliona uhitaji wa vituo vya afya, shule na vituo vya kulelea watoto katika maeneo ya ukombozi ili kuhudumia watoto waliokuwa wakipoteza wazazi kutokana na vita.

1969 ulikua mwaka mzuri kwa Josina.  Aliteuliwa kuwa mkuu wa Idara ya Mambo ya uhusiano ya FRELIMO nafasi ambayo ilimfanya awe anatembea kwenda nchi mbalimbali kwenye mikutano iliyohusu haki za wanawake.

Ambapo aliendeleza kwa bidii vituo vya utunzaji wa watoto kaskazini mwa Msumbiji (Cabo Delgado ) na kutetea watu wa eneo hilo bila kusahau kuwafundisha umuhimu wa kupeleka wasichana shuleni. Wakati ambao Rais wa FRELIMO EDUARDO MONDLANE anauawa nchini Tanzania na maajenti wa kireno ili kudhorotesha harakati za ukombozi.

Josina alikuwa mtetezi wa wanawake kiuchumi, kijamii na kielimu. Alifunga ndoa na Samora katika Kituo cha Mafunzo cha wilaya ya Tunduru kusini mwa Tanzania. Novemba mwaka huo alijifungua mtoto wao wa kiume, Samito AKA Samora Jr
Mwaka 1970 Josina alianza kupata maumivu ya tumbo na kuwa dhaifu ki afya. Alisafiri na kwenda Moscow kwa matibabu na kuonekana ana saratani ya ini. Alitakiwa kupumzika lakini Josina alirudi kwenye majukumu yake na FRELIMO.

Mwisho wa mwaka, alimuacha Samito na rafiki yake na kuchukua safari ya miezi miwili ambapo kwa kiasi kikubwa alitembea kwa miguu kupitia Mkoa wa Niassa kukagua hali na kupanga shughuli mbalimbali kwenye idara yake.

Mnamo Machi 1971 Josina alisafiri tena, wakati huu alikwenda Cabo Delgado, kukagua mipango ya kijamii inayotekelezwa huko. Kwa wakati mmoja alifanya kikao na watu zaidi ya 1000 akiwa mchovu na dhoofulhalia. Hapo anaamua kurudi Dar es salaam mwanzoni mwa Aprili. Wakati anavuka mpaka wa Tanzania, alikabidhi bastola yake kwa mwenzake na kumwambia "Wenzangu, siwezi kuendelea tena. Toa hii kwa kamanda wa jeshi ili iweze kuchangia wokovu wa watu wa Msumbiji. "

Aprili 5 Josina alikua na hali mbaya mkoani Dar es salaam. Alipelekwa katika Hospitali ya Muhimbili ila alifariki mnamo Aprili 7, 1971 akiwa na miaka 25. Chama cha FRELIMO kiliitangaza siku hii kuwa siku ya kitaifa ya wanawake Msumbiji. Ilikuwa ni miaka minne baadae ambapo uhuru ulipatikana. Alizikwa kwenye kaburi la Kinondoni ambapo alizikwa karibu na mjomba wake Mateus Muthemba, aliyeuliwa na mawakala wa Ureno mnamo 1968.


Mwaka 1972, ikiwa ni mwaka mmoja baada ya Josina kufariki dunia, mmoja wa viongozi wa Frelimo, Oscar Monteiro, alimtaja Josina kama kamanda muhimu wa Frelimo na Msumbiji aliyeangukia njiani. Kauli hiyo ilimfanya Samora aanguke chini na kulia.

Samora aliandika shairi kumlilia Josina: “Yaani zaidi ya mke, ulikuwa dada kwangu, rafiki na kamanda katika jeshi. Tunawezaje kumuomboleza kamanda, lakini kuchukua bunduki iliyoanguka na kuendelea kupigana. Machozi yangu yanatiririka kutoka pale kwenye chanzo kilichozaa penzi letu, nia yetu na mapinduzi ya maisha yetu.”

Post a Comment

0 Comments