HISTORIA/SHUJAA :Yaa Asantewaa, AFRIKA NA UAFRIKA VOL 1

Ni ajabu sana hii dunia ilivyoumbwa, umewahi ona wanawake wapambanaji? Mwanamziki kutoka Kingstone Jamaica Orville Richard almaarufu kama Shaggy, ana nyimbo yake ambayo amemwelezea mwanamke alivyo na nguvu na upendo. 

Mwanamke akikaa sehemu basi lazma mambo yanyooke.. kama utahitaji kujadili kuhusu hili me nipo tayari kukupa mifano ya wanawake wenye sifa hizo.
Dr Hellen Kijo Bisimba nimekupa, Wangari Mathai kutoka Kenya nimekupa, Bibi Zura Karuhimbi kutoka Rwanda nimekupa 

na leo nakupa ya Yaa Asantewaa.
Yaa Asantewaa alikuwa malkia mashuhuri wa Ashanti mwanzoni mwa karne ya ishirini ambaye bado ni ishara ya nguvu mpaka leo hii. Inasadikika alizaliwa kati ya miaka ya 1840 hadi 1860 huko Ashanti  ambapo ndio Ghana ya leo. Alikuwa mkulima mzuri kabla ya kuwa mama Malkia mnamo miaka ya 1880. Inaaminika kuwa alichaguliwa na kupewa cheo hiki na kaka yake mkubwa Nana Akwasi Afrane Okpase, ambaye alikuwa mtawala mwenye nguvu wakati huo.

Kama Mama Malkia, Asantewaa alishikilia majukumu mengi, ikiwa ni pamoja na kuwa mlinzi wa kiti cha dhahabu. Kiti cha dhahabu ni ishara ya ufalme wa Ashanti, mfumo wa kitamaduni, na nguvu. Yeye ndiye anakuwa mshauri mkuu wa Mfalme, na kuifanya nafasi yake kuwa ya pili kicheo kutoka kwa mfalme na ni jukumu lake kukilinda kiti hiko.

Mnamo 1896, watu wa Ashanti walianza kupambana na muingereza katika nchi yao ikiwa ni jaribio la Uingereza kujenga koloni katika nchi ya Ghana. Ili kulipiza kisasi, Waingereza walimteka na kumfukuza Asantehene Prempeh I, Mfalme wa Ashanti na mjukuu wa Asantewaa Kofi Tene, ambaye pia alikuwa kiongozi mwenye nguvu. Waingereza waliondoa mfalme na viongozi wengine wa Ashanti na kuwapeleka Visiwa vya shelisheli ili waweze kupata kiti cha dhahabu.
Sir Frederick Hodgson wa Gold Coast alifikiri ya kwamba ugumu wa kutawala Waashanti ungepungua kama yeye mwenyewe angeshika kiti cha dhahabu. Wanajeshi aliotuma kukitafuta walishindwa. Hivyo gavana Hodgson mwenyewe alienda Kumasi akaita mkutano wa watawala wa maeneo ya Ashanti akadai kupewa kiti cha dhahabu na malipo ya kodi.

Hotuba ya gavana ilikasirisha viongozi lakini waliondoka kimya. Yaa Asantewaa alishiriki na kabla ya mkutano alionekana kumtania gavana kwa kusimama mbele yake na kuangalia nishani kwenye sare yake kwa muda mrefu.
Baada ya kusikia madai ya gavana alimpinga kwa kumwambia hastahili kupata kiti cha dhahabu na akikitaka amrudishe Asantehene anayejua maficho ya kiti hiko.

Walikutana baadaye kati yao wakishauriana namna gani kujibu mapigo ya mwingereza. Yaa Asantewaa Alipoona ya kwamba sehemu ya viongozi walitaka kunyamaza alitoa hotuba akiwauliza wakuu wengine namna gani waliweza kunyamaza tu na kuyanyamazia maneno ya Mwingereza, na kama wameacha kuwa wanaume ili wabadilishwe kuwa wanawake? Asantewaa alitangaza kwamba ikiwa wanaume wa ufalme hawatatetea watu, basi wanawake wataibuka. Hee kauli nzito hizi, ukitaka kuona nguvu za wanaume toa kauli kama hizi.
Katika mkutano huu Yaa Asantewaa alichaguliwa kuwa kiongozi wa vita wa Ashanti. Asantewaa alishikilia msimamo wake na kuwasaidia askari. Alisimama kama Kamanda  Mkuu wa jeshi la Ashanti. Na kupelekea  vita vya tano na vita vya mwisho vya Anglo-Ashanti dhidi ya muingereza vilivyojulikana kama Vita vya Uhuru vya Yaa Asantewaa (au Vita vya kiti cha Dhahabu), ambavyo vilianza Machi 28, 1900.

Yaa Asantewaa aliongoza uasi ambao ulisababisha vifo cha wanajeshi 1,000 wa Uingereza na washirika wa Kiafrika na Ashanti 2000.Hii ilikua idadi kubwa kuwahi kutokea katika vita vyote ambavyo vilipita .

Vita iliendelea hadi Julai ambapo Waingereza walikusanya jeshi jipya kutoka vikosi vyao vya Sierra Leone na Nigeria na jeshi hili lilifika Kumasi kwenye Julai na kufukuza jeshi la Waashanti. Katika miezi iliyofuata walishinda upinzani wote.

Yaa Asantewa ni mfano muhimu na msukumo kwa wasichana na wanawake wengi nchini Ghana na afrika kwa ujumla kwasababu ya ujasiri aliouonyesha. Wanawake wengi ambao wanafanya kazi ambazo hapo awali zilikuwa zikitawaliwa na wanaume mara nyingi wamepewa jina la Yaa Asantewaa ikiwa ni njia ya kuwatia moyo na kuwaunga mkono.
Mnamo mwaka 2000, makumbusho moja ilijengwa kwa kumbukumbu ya malkia huyo wa vita huko Ejisu. Familia yake ilikuwa na ukarimu wa kutosha kuchangia vitu maalum vya urithi na vitu ambavyo Yaa Asantewaa alivitumia, ikiwemo nguo, gamba la kobe ambalo inaaminika alikuwa akitumia kulia chakula. Kwa bahati mbaya, makumbusho hayo yaliungua kwa moto Julai 2004. Vitu vingi vilipotea na makumbusho hayo yamesalia tupu.

Post a Comment

0 Comments